Saturday, July 11, 2020

AMREF WATOA MSAADA WA VIFAA KINGA KWA AJILI YA TAHADHARI YA CORONA SIMIYU



Shirika lisilo la Kiserikali la AMREF kupitia mradi wa UZAZI UZIMA limetoa msaada wa vifaa kinga kuunga mkono Serikali katika tahadhari dhidi ya maambukizi ya Virusi vya CORONA kwa mkoa wa Simiyu.

Akikabidhi vifaa hivyo vyenye thamani ya zaidi ya shilingi millioni 23, Mratibu wa AMREF Kanda ya Ziwa, Bw. Gaspery Misungwi Julai 09, 2020 Mjini Bariadi, amesema Shirika hilo linatambua kazi kubwa iliyofanywa na Serikali katika mapambano dhidi ya Corona hivyo kama wadau wameona waungane na serikali katika kutokomeza kabisa janga hilo.

Aidha, Bw. Misungwi amevitaja vifaa hivyo kuwa ni pamoja na mmipira ya kuvaa mikononi wakati wa kutoa huduma kwa wagonjwa, barakoa,vitakasa mikono (ujazo tofauti), sabuni za maji za kunawia mikono(ujazo tofauti) na ndoo kwa ajili ya kunawia mikono.

Akipokea msaada huo, Katibu Tawala wa Mkoa, Bi. Miriam Mmbaga amelishukuru shirika hilo kwa msaada huo huku akibainisha kuwa vifaa kinga hivyo havitatumika katika tahadhari dhidi ya corona peke yake maana utakasaji unazuia magonjwa mengi.

Mmbaga ameongeza kuwa mkoa wa Simiyu uko tayari kufanya kazi kwa kushirikiana na wadau wote kwa kuzingatia sheria kanuni na taratibu za Serikali kwa kuwa nia ya serikali ni kurahisisha utoaji huduma kwa wananchi.

Katika hatua nyingine Mmbaga ameelekeza vifaa hivyo vipelekwe katika maeneo yaliyokusudiwa na wala visipelekwe stoo.

Kwa upande wake Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa, Dkt. Khamis Kulemba amesema pamoja na AMREF kutoa vifaa kinga hivyo shirika hilo limekuwa likisaidia katika ujenzi wa miundombinu hususani majengo ya upasuaji katika baadhi ya vituo, uchimbaji wa visima Vya maji na katika huduma za afya ya mama na mtoto.

Dkt. Kulemba ameongeza kuwa kwa ushirikiano kati ya AMREF na serikali hali ya mahudhurio ya wakina mama wajawazito kuhudhuria kliniki imeongezeka kufikia asilimia 80 na wanawake kujifungulia katika vituo Vya kutolea huduma za afya.
MWISHO
Mratibu wa AMREF Kanda ya Ziwa, Bw. Gaspery Misungwi (wa pili kulia) akikabidhi msaada wa vifaa kinga kwa ajii ya tahadhari ya maambukizi ya virusi vya Corona mkoani Simiyu kwa Katibu Tawala wa mkoa huo, Bi. Miriam Mmbaga(wa pili kushoto) Julai 09, 2020 Mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!