Thursday, May 3, 2018

MWALIMU ALIYETOA ALAMA A 90 MTIHANI WA DARASA LA SABA 2017 APEWA TUZO MKOANI SIMIYU



Mwalimu Akwilina Ernest Marenge kutoka Shule ya Msingi Salunda katika Halmashauri ya Mji wa Bariadi Mkoani Simiyu, amepata zawadi ya shilingi 500,000/= kwa ajili ya pongezi kwa kufanikiwa kutoa Alama A kwa wanafunzi 90 kati ya wanafunzi 147 katika Somo la Kiswahili katika mtihani wa Darasa la Saba mwaka 2017.

Fedha hizo zimetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka kwa mwalimu huyo mbele ya baadhi ya viongozi wa mkoa huo, wanafunzi  na walimu wengine wa Shule ya Msingi Salunda.

Akikabidhi fedha hizo Mtaka amesema Serikali imetambua juhudi za mwalimu huyo ambaye  Katika somo lake la Kiswahili alikuwa na ufaulu mzuri ambapo alitoa alama A 90, Alama B 55 na Alama C 2, hivyo kama kiongozi ameona ni vema mwalimu huyu akapewa motisha.

"Siku ya Mei Mosi alipewa shilingi laki tano kama mfanyakazi hodari na mimi nikasema nitampa shilingi 500,000 za kwangu siyo za Serikali, kama kiongozi niliona ni jambo  la kupongezwa, Fedha hii haifanani na alichofanya kwa watoto ila najua wanafunzi wake watamkumbuka daima" alisema Mtaka.

Kwa upande wake Mwl. Akwilina Marenge ambaye anatarajia kustaafu mwezi Juni mwaka 2018 amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka kwa kutambua juhudi zake na kuona umuhimu wa kumpongeza na akatoa wito kwa walimu wengine kujituma na kupenda kazi yao.

Nao Walimu wenzake na Mwalimu Akwilina  wamempongeza na kubainisha kuwa anastahili kupata zawadi zote hizo kwa kuwa pamoja na kuwa umri mkubwa  amekuwa ni mtu wa kujituma na kufanya kazi kwa bidii zaidi ya walimu vijana.

"Mwalimu Akwilina ni mwalimu wa tofauti na walimu wengine, pamoja na kwamba yeye umri wake umekwenda sana anawahi kazini, anaipenda kazi yake, anajituma kuliko hata walimu vijana, ni mcheshi; hata sasa hivi tunavyosikia anaenda kustaafu tunasikitika kwa sababu anaondoka mtu mchapakazi" alisema mwalimu Tabitha Erasto.

" Huyu mama ni mtu mzima lakini anajituma kuliko baadhi ya walimu vijana ni kitu cha kushangaza mno,  japo anaelekea kustaafu sisi  wenzake tunaobaki tunapaswa tuige mfano wake kwa kweli" Alisema Mwalimu Joyce Mishana.

Akitoa shukrani kwa niaba ya walimu wengine Mwalimu Mkuu wa Shule ya Salunda, Mwl. Nchambi Tupendane amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Simiyu kwa kutambua mchango wa mwalimu Akwilina na kubainisha kuwa zawadi hiyo imekuwa ni chachu kwao ya kufanya vizuri zaidi katika Mtihani wa Taifa mwaka huu na miaka ijayo.

Kutokana na utendaji kazi mzuri Mwalimu Akwilina pia alitambuliwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi kuwa Mfanyakazi Hodari na siku ya Mei Mosi  alizawadiwa shilingi laki tano na cheti.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (mwenye suti katikati) akimkabidhi  Mwalimu Akwilina Marenge wa Shule ya Msingi Salunda fedha taslimu shilingi  500,000 kwa ajili ya pongezi kwa kutoa alama A kwa  wanafunzi 90 kati 147 katika somo la Kiswahili, Mtihani wa Taifa wa Darasa la Saba mwaka 2017.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka (kulia) akimkabidhi  Mwalimu Akwilina Marenge wa Shule ya Msingi Salunda fedha taslimu shilingi  500,000 kwa ajili ya pongezi kwa kutoa alama A kwa  wanafunzi 90 kati 147 katika somo la Kiswahili, Mtihani wa Taifa wa Darasa la Saba mwaka 2017.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Msingi Salunda wakishuhudia mwalimu wao akipokea fedha taslimu shilingi  500,000 kwa ajili ya pongezi kwa kutoa alama A kwa  wanafunzi 90 kati 147 katika somo la Kiswahili, Mtihani wa Taifa wa Darasa la Saba mwaka 2017.


Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Salunda, Nchambi Tupendane akionesha fedha alizopokea kutoka kwa Mkuu wa Mkoawa Simiyu kwa ajili ya walimu wa shule hiyo kujipongeza pamoja na mwalimu mwenzao kwa kutoa ufaulu mzuri katika somo la Kiswahili, Mtihani wa Taifa wa Darasa la Saba mwaka 2017.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!