Tuesday, May 8, 2018

TRA KUANZISHA VITUO VYA ELIMU NA HUDUMA KWA WALIPAKODI



Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatarajia kuanzisha vituo vya Elimu na huduma kwa walipakodi  hivi karibuni, ambavyo vitawasaidia walipakodi kupata ushauri wa masuala ya kodi pamoja na kujua haki na wajibu wao.

Hayo yamesemwa na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania Charles Kichere  Mjini Bariadi, wakati akizungumza na wafanyabiashara, Viongozi na watendaji wa Wilaya na Mkoa  Mkoani  Simiyu, wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili kwa Walipakodi mkoani humo.

Kamishna Kichere amesema uamuzi wa TRA  wa kuanzisha vituo hivyo umelenga kusogeza huduma karibu kwa walipakodi ambapo wafanyabiashara(walipakodi)  watapata huduma za ushauri kuhusu masuala ya kodi bila malipo katika vituo hivyo vitakavyokuwa nje ya Ofisi za TRA.

“Tunajua elimu ni muhimu sana kwa walipakodi wetu, tunataka itolewe kwa walipa kodi kila siku siyo kwa misimu; ili kusogeza huduma karibu hivi karibuni tutaanzisha vituo vya Elimu na Huduma kwa walipakodi nje ya TRA, ambavyo vitatoa huduma ya ushauri kwa walipakodi bure” alisema Kichere

Aidha, Kichere ametoa wito kwa Wafanyabishara wa Mkoa wa Simiyu ambao ameutaja kama mkoa wenye fursa nyingi za kibiashara kujitokeza kwa wingi kujisajili katika vituo  vya elimu na usajili wa walipakodi, kupitia zoezi linaloendelea mkoani humo ambalo limezinduliwa rasmi na Mkuu wa Mkoa huo, Mhe.Anthony Mtaka, Mei 08, 2018.

Ameongeza kuwa ni vema wafanyabiashara wakatambua umuhimu wa kulipa kodi stahiki kwa wakati stahiki, ili Serikali iendelee kutoa huduma bora kwa wananchi kupitia kodi hizo na akasisitiza wafanyabiashara ambao bado hawajarasimisha biashara zao wajisajili na kuanza kulipa kodi .

Wafanyabishara wa Mkoa wa Simiyu wameipongeza Mamlaka ya Mapato Tanzania Mkoa wa Simiyu kwa kufanya nao kazi kwa ushirikiano na wakaomba changamoto mbalimbali zilizopo kufanyiwa kazi ili waweze kutimiza wajibu wao kikamilifu kama walipakodi.

“ Tunaomba Ofisi ya Mkoa ya TRA iboreshwe iendane na hadhi ya Mkoa, Wilaya zetu mpya za Busega na Itilima ziwe na Ofisi za TRA ili kuwaondolea wafanyabiashara wenzetu shida ya kufuata huduma katika wilaya nyingine na pia wafanyabiashara tunahitaji elimu ya mara kwa mara kwenye masuala ya kodi” alisema Christina Matulanya Katibu wa TCCIA Simiyu.

“Tunaomba TRA waziangalie upya sheria zao, lakini pia waangalie viwango vya kodi wanavyowakadiria  wafanyabiashara ili viendane na hali halisi ya biashara za Watanzania tulio wengi” alisema Davis Mateko Mfanyabiashara kutoka Wilaya ya Busega.

Akizindua kampeni ya Elimu na Usajili kwa walipakodi , Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka ameiomba TRA kutatua changamoto za mashine za kutolea risiti (EFD), huku akitangaza dhamira yake ya kuona biashara zinafanyika saa 24 katika Makao Makuu ya Wilaya na Baadhi ya Vituo (Centres) vikubwa  kuiwezesha TRA kukusanya kodi zaidi.

Katika hatua nyingine Mtaka amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri Mkoani humo kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli la kuzingata maeneo ya wafanyabiashara wadogo wakati wa Ujenzi wa Vituo vya Mabasi na akasisitiza wafanyabiashara wadogo kujisajili ili waweze kupewe kipaumbele vituo hivyo vitakapojengwa.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka (wa pili kushoto)  akikata utepe kuashiria Uzinduzi wa Kampeni ya  Elimu na Usajili wa Walipakodi  Mkoani humo leo Mjini Bariadi,  ambayo inaendeshwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Kamishna Mkuu TRA , Bw. Charles Kichere akizungumza na Viongozi  na Watendaji wa Serikali pamoja na Wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu, wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani humo ambao umefanyika leo mjini Bariadi.

Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi TRA  Bw. Richard Kayombo akizungumza na Viongozi  na Watendaji wa Serikali pamoja na Wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu, wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani humo ambao umefanyika leo mjini Bariadi.



Katibu wa Chama cha Wafanyabiashara(TCCIA) Mkoa wa Simiyu, Bibi. Christina Matulanya akichangia hoja mbele ya wafanyabiashara wenzake wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani humo ambao umefanyika leo mjini Bariadi.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na Viongozi  na Watendaji wa Serikali pamoja na Wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu, wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani humo ambao umefanyika leo mjini Bariadi.


Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Bw.Jumanne Sagini akizungumza na Viongozi  na Watendaji wa Serikali pamoja na Wafanyabiashara wa Mkoa wa Simiyu, wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani humo ambao umefanyika leo mjini Bariadi.


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akipata maelezo kutoka kwa Afisa wa TRA kuhusu namna Wafanyabiashara  watakavyokuwa wakisajiliwa , mara baada ya Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani humo ambao umefanyika leo mjini Bariadi.


Mfanyabiashara Gungu Emmanuel Silanga akichangia hoja mbele ya wafanyabiashara wenzake wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani Simiyu  ambao umefanyika leo mjini Bariadi.


Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara Wilaya ya Busega, Bw.Davis Mateko akichangia hoja mbele ya wanyabiashara wenzake wakati wa Uzinduzi wa Kampeni ya Elimu na Usajili wa Walipakodi Mkoani Simiyu  ambao umefanyika leo mjini Bariadi.






0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!