Saturday, May 5, 2018

SERIKALI YATOA VITABU 297,891 KWA SHULE ZA MSINGI MKOANI SIMIYU



Serikali imetoa jumla ya Vitabu 297, 891 kwa ajili ya wanafunzi wa Shule za Msingi wa Darasa la kwanza mpaka darasa la Tatu Mkoani Simiyu

Akizungumza kabla ya makabidhiano ya vitabu hivyo Mwakilishi kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Ndabazi Stephano amesema vitabu hivyo vitakidhi mahitaji  ya wanafunzi kwa kuwa idadi yake ni kubwa zaidi ya idadi ya wanafunzi wa darasa la kwanza hadi la tatu ambao wako 261,257 kwa mkoa mzima.

Amesema  azma ya Serikali ni kuhakikisha kuwa kila shule ina vitabu vinavyojitosheleza na inaendelea kuchapisha  vitabu vya darasa la nne, ambapo Ofisi ya Rais TAMISEMI  imeanza kugawa vitabu hivyo katika mikoa mbalimbali na akabainisha kuwa mkoa wa Simiyu nao utapewa vitabu hivyo.

"Tunaendelea kugawa vitabu vya darasa la nne katika mikoa mbalimbali hapa nchini, hadi sasa vimegawanywa katika mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Lindi, Mtwara, Ruvuma, Njombe, Iringa, Dodoma, Morogoro na awamu inayokuja ni Mikoa ya Kanda ya Ziwa ukiwemo Simiyu” alisema Stephano.

“Vitabu hivi ni original  (halisi) kabisa hamna kitabu feki hapa, maana kuna taarifa zinasambaa mitandaoni kuwa vitabu hivi vimekosewa,  niwaeleze walimu na wanafunzi mliopo hapa vitabu hivi tunavyovigawa ni halisi na  havijakosewa” alisisitiza Ndabazi Stephano

Aidha, Bw.  Gaitan Romwald kutoka Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) amesema vitabu hivi vinagawiwa kwa awamu, hivyo vipo vitabu vingine vya darasa la kwanza mpaka la tatu ambavyo kwa Mkoa wa Simiyu vitagawiwa pamoja na vitabu vya darasa la nne awamu ijayo.

Akizungumza na walimu na wanafunzi walioshuhudia makabidhiano ya vitabu hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amewataka wanafunzi kuvitunza na kuvisoma ili viwasaidie katika masomo yao,  huku akiwataka walimu kuvitumia vitabu hivyo kuwafundisha wanafunzi kwa moyo.

Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Julius Nestory ameishukuru Serikali kwa kuleta vitabu hivyo ambavyo amesema vitatatua tatizo la upungufu wa vitabu uliokuwepo kutokana na ongezeko la wanafunzi wanaoandikishwa mwaka hadi mwaka.

Walimu na wanafunzi pia wameishukuru Serikali kwa kupeleka vitabu hivyo Mkoani Simiyu ambavyo vitakuwa chachu  na njia mojawapo ya kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia.

“Tunaishukuru sana Serikali kwa kuleta hivi vitabu, vitatusaidia katika masomo yetu maana tutajisomea ili tujifunze na kupata uelewa zaidi" Eliasi John mwanafunzi Shule ya Msingi Somanda A

“Kwa niaba ya walimu wenzangu na wanafunzi wetu, napenda kuishukuru Serikali kutuletea vitabu hivi, vitakuwa msaada mkubwa sana kwa wanafunzi wetu lakini hata kwetu pia na vitatusaidia sana kuboresha mazingira yetu ya kufundishia watoto” Mwalimu Janeroza Gabriel

MWISHO
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka(mwenye suti ya bluu)  na baadhi ya walimu na wanafunzi wa Shule ya Msingi Somanda A na B Mjini Bariadi, wakipokea vitabu vilivyoletwa na Serikali kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani humo,  (wa tatu kulia) Ndabazi Stephano kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI na (wa nne kulia) Gaitan Romwald  kutoka Mamlaka ya Elimu Tanzania, kulia Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Julius Nestory.

Sehemu ya sehena ya vitabu 297, 891 vilivyoletwa na Serikali kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani Simiyu vikiwa vimeandaliwa tayari kwa kupelekwa katika Halmashauri Mkoani humo ili viweze kupelekwa katika shule zote za msingi.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka akizungumza na Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Msingi Somanda A na B Mjini Bariadi, mara baada ya kupokea vitabu vilivyoletwa na Serikali kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani Simiyu(havipo pichani).


Afisa Elimu wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Julius Nestory akizungumza na Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Msingi Somanda A na B Mjini Bariadi,  mara baada ya kupokea vitabu vilivyoletwa na Serikali kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani Simiyu(havipo pichani).


Mwl. Gaitan Romwald  kutoka Mamlaka ya Elimu Tanzania(TEA) akizungumza na baadhi ya viongozi wa Mkoa wa Simiyu pamoja na Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Msingi Somanda A na B Mjini Bariadi, mara baada ya kukabidhi  vitabu vilivyoletwa na Serikali kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani humu(havipo pichani).


Bw. Ndabazi Stephano kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI akizungumza na baadhi ya viongozi wa Mkoa wa Simiyu pamoja na Walimu na Wanafunzi wa Shule ya Msingi Somanda A na B Mjini Bariadi , mara baada ya kukabidhi  vitabu vilivyoletwa na Serikali kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani humo(havipo pichani).

Mwanafunzi Buguma Nindwa wa Shule ya Msingi Somanda B akizungumza na waandishi wa habari  (hawapo pichani)  mara baada ya kushuhudia makabidhiano ya vitabu vilivyoletwa na Serikali kati ya wawakilishi wa Wizara ya Elimu, Ofisi ya Rais TAMISEMI na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, mhe.Anthony Mtaka  kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la kwanza mpaka darasa la tatu mkoani humo.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!