Wednesday, August 5, 2020

WAZIRI HASUNGA AONGEZA SIKU MBILI MAONESHO YA NANENANE 2020

Kutokana  na kuchelewa kuanza kwa maonesho ya Nanenane Mwaka 2020 katika baadhi ya kanda serikali imetangaza kuongeza siku mbili za maonesho hayo ambapo kwa mwaka huu yatahitimishwa Agosti 10 badala ya Agosti 8.

Taarifa hiyo imetolewa Agosti 04, 2020 na  Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga wakati alipotembelea Banda la Chama cha wajasariamali wanawake Tanzania (TABWA) kwenye viwanja vya Maonesho ya wakulima (Nanenane) ambayo kitaifa yanafanyika Nyakabindi Mkoani Simiyu.

Hasunga amesema kuwa kulingana na mahitaji ya wadau mbalimbali na wananchi kuendelea kujifunza mbinu bora za kilimo hususani ambao hawakupata fursa awali watatumia siku hizo zilizoongezwa katika kanda zote kujionea mbinu bora za kilimo, mifugo na uvuvi na teknologia za kisasa.

“Awali tulipanga kufanya maonesho ya nanenane mwaka 2020 siku nane lakini  kutokana na maombi ya wadau na wananchi pamoja na baadhi ya kanda kuchelewa kufungua maonesho haya,  kwa mamlaka niliyopewa natangaza rasmi leo kuongeza siku mbili za maonesho, kwa hiyo tutahitimisha Agosti 10, 2020” alisema Hasunga.

Wakati huo huo mhe. Hasunga amewataka wananchi wote nchini, wakiwemo wafugaji, wavuvi na wakulima kutumia fursa hiyo ya siku zote 10 za maonesho kwenda kujifunza zaidi, teknologia mpya za kilimo, uvuvi na ufugaji.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Bariadi Festo Kiswaga akizungumzia kuongezwa muda wa maonesho ya nane nane alisema  amelipokea vizuri tamko hilo na  watazitumia vizuri siku hizo zilizoongezwa hasa kujifunza mambo ambayo wasingeweza kuyapata pasipo kuongezewa muda huku akitoa rai kwa wakulima kujitokeza kwa wingi kufika kwenye maonesho hayo kujifunza teknolojia mbalimbali .

 

Kwa upande wake Luteni Kanali Peter Lushika ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya nane nane katika Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) akizungumza kwa niaba ya washiriki wa maonesho hayo alisema kuwa wamefurahia agizo hilo ambalo limewapa fursa ya kuendelea kutoa elimu kwa wakulima, wafugaji na wavuvi ambao hawajapata fursa hiyo.

 Aidha Luteni  Kanali Lushika ametoa rai kwa wananchi kutembelea banda lao kujifunza teknolojia nyingi ambazo Jeshi hilo limeandaa hatua itakayowawezesha kubadilisha mfumo wa utendaji kazi zao hatua ambayo itawasaidia kuongeza thamani kwenye mazao yao.

 Aliyekuwa katibu tawala wa Mkoa wa Simiyu Jumanne Sagini amesema kuwa maonesho ya mwaka 2020 yana maboresho makubwa ya mazao na teknolojia nyingi huku akitoa rai kwa wananchi kutembelea viwanja hivyo ili kupata elimu itakayowaletea kuboresha shughuli zao za Kilimo, Mifugo na Uvuvi hatua ambayo itapelekea kuongeza tija kwenye shuguli zao.

MWISHO 

Waziri wa Kilimo, Mhe. Japhet Hasunga(wa pili kulia) akitoa taarifa ya kuongeezwa kwa siku mbili za maonesho ya nanenane, Agosti 04, 2020 kulia Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!