Tuesday, July 2, 2019

MAKAMPUNI 12 KUANZA KUNUNUA PAMBA KWA BEI ELEKEZI 1200


Baada ya kikao kati ya Viongozi wa Mkoa wa Simiyu na wadau wa pamba mkoani Simiyu jumla ya makampuni 12 yamekubali kuingia sokoni kunua pamba ya wakulima kwa bei elekezi ya shilingi 1200.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka wakati wa kufunga kikao maalum cha kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba katika mkoa wa Simiyu, ambapo pia ilielekezwa kuwa makampuni yaliyokubali kununua pamba kwa wakulima yazingatie sheria na taratibu na yawalipe wananchi fedha zao  kwa wakati.

Mtaka ameyapongeza makampuni yote yaliyokubali kuingia kununua pamba huku akiahidi kutoa msaada kwa wafanyabiashara wanaokutana na changamoto ya upatikanaji wa fedha kutoka katika taasisi za fedha na kuwahakikishia kuwa kila atakayehitaji msaada atamsaidia ili apate fedha.

Aidha, Mtaka amesema yeyote atakayebainika kufanya udanganyifu katika mizani achukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria huku akiutaka wakala wa vipimo kusimamia na kuhakikisha mizani hazichezewi katika Vyama vya Ushirika vya Msingi(AMCOS).

“ Kama kuna wakati Wakala wa Vipimo unahitaji kuwa na saa nyingi za kufanya kazi ni sasa kama magari hayatoshi waombe tutawapa na kama watumishi hawatoshi omba watalaam kutoka katika maeneo mengine, kama kuna mtu atakutwa amefanya udanganyifu katika mizani kwenye vyama vya ushirika achukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria” alisema Mtaka.

Kwa upande wao Wanunuzi wa pamba mkoani SIMIYU wameiomba serikali kuondoa tozo zote zilizopo kwenye utaratibu wa ununuzi wa pamba, ili kupunguza hasara watakayopata kwa kununua pamba kwa Bei elekezi ya shilingi 1200 kwa kilo kutokana na bei ya soko la dunia kushuka, jambo ambalo lililofafanuliwa na Katibu Tawala Mkoa, Bw.Jumanne Sagini kuwa tozo hizo ni jambo la kisera na kisheria nchini hivyo haliweze kufanyiwa maamuzi na mkoa.

Katika hatua nyingine baadhi ya wanunuzi wa pamba wakapendekeza  kuanzishwa kwa  viwanda vya nyuzi na nguo ili kuongeza thamani ya Pamba na kuondokana na utegemezi wa bei  ya soko la dunia.

“Tukisema mwaka huu tutoe tozo fulani na mwakani tutatoa nyingine tena, hiyo haitakuwa tiba kwenye bei ya soko la dunia, Tiba pekee ya kulinusuru zao la pamba ni kuwekeza kwenye viwanda vya nyuzi na nguo na hilo tunaliweza, tuwekeze sisi Wanasimiyu viwanda vijengwe Simiyu” alisema Mnunuzi wa Pamba Gungu Silanga.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe, Festo Kiswaga amewataka wanunuzi wote kuzingatia sheria wakati wakinunua pamba ya wakulima na akasisitiza kuwa wale watakaokiuka sheria ikiwa ni pamoja na kununua pamba usiku watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria.

Baadhi ya Makampuni yaliyokubali kuingia kununua pamba mkoani Simiyu ni pamoja na Alliance Ginneries Limited, NGS, MWATEX, GAKI, OLAM, SM na Vitrex
MWISHO
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na wadau wa zao la pamba mkoani hapa, kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na wadau wa zao la pamba mkoani hapa, kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.
Gungu Silanga mnunuzi wa pamba mkoani Simiyu akichangia hoja katika kikao cha wadau wa pamba mkoani Simiyu kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.
Mkuu wa Wilaya ya Itilima Mhe. Benson Kilangi akichangia hoja katika kikao cha wadau wa pamba mkoani Simiyu kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.



 Mnunuzi wa Pamba mkoani Simiyu, Bw. Malongo Midimu  akichangia hoja katika kikao cha wadau wa pamba mkoani Simiyu kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.

 Katibu wa chama cha Wanunuzi wa Pamba nchini, Bw. Boaz Ogola akichangia hoja katika kikao cha wadau wa pamba mkoani Simiyu kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meatu, Bw. Fabian Manoza akichangia hoja katika kikao cha wadau wa pamba mkoani Simiyu kilicholenga kujadili mstakabali wa ununuzi wa pamba mkoani hapa, kilichofanyika Mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!