Wednesday, September 5, 2018

CHAMA CHA USHIRIKA SIMIYU CHAFANYA UCHAGUZI KWA MARA YA KWANZA, VIONGOZI WAASWA KUENDESHA USHIRIKA KISASA


Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu- Simiyu Co-Operative Union (SIMCU) kimefanya Uchaguzi wa Viongozi wa Chama hicho, ikiwa ni kwa mara ya kwanza kwa Chama hicho kufanya Mkutano wake Mkuu, tangu kuanzishwa kwake baada ya Simiyu kujitoa Uanachama kwenye Vyama vya Ushirika  vya NYANZA  na SHIRECU.

Katika Mkutano huo uliofanyika  Mjini Bariadi Septemba 04, 2018, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka amewataka viongozi waliochaguliwa kuendesha ushirika wa kisasa ambao utakuwa wa tofauti huku akihimiza SIMCU kuwekeza katika maendeleo ya elimu, afya na ujenzi wa vitega uchumi.

“Viongozi vaeni mawazo ya kisasa muendeshe Ushirika kisasa, ningependa kuona Chama chetu cha Ushirika cha mkoa(SIMCU) kinajipambanua kwenye maendeleo hasa elimu na afya; wekezeni katika kujenga vitega uchumi, haiwezekani mkusanye zaidi ya bilioni moja kutokana pamba kwenye AMCOS halafu mkashindwa kujenga vitega uchumi” alisema Mtaka.

Naye Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Dkt. Titus Kamani amewaasa viongozi wa SIMCU pamoja na vongozi wa Vyama vya Ushirika vya msingi (AMCOS) kusimamia ushirika mkoani humo kwa uadilifu na kuiacha historia ya zamani ambayo baadhi ya viongozi walichukulia ushirika kama mahali pa kupiga dili na mali isiyo na mwenyewe.

Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Simiyu(SIMCU), Bw. Charles Madata, amesema atahakikisha SIMCU inafanya mambo ya maendeleo kama Mkuu wa Mkoa huo alivyosema, ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika elimu, afya, kujenga vitega uchumi na kusimamia Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) ili vijiendeshe kibiashara.

Aidha, Madata amebainisha mikakati yake mingine kuwa ni kusimamia nidhamu ya matumizi ya  fedha na mali za Ushirika, kutafuta soko la pamba ndani na nje, ili bei ya pamba iweze kupanda na kufikia zaidi ya shilingi 1500/= na kuwahamasisha wakulima kujiunga na ushirika ili kuboresha maisha yao.

Nao wanachama wa Vyama vya Ushirika vya Msingi (AMCOS) ambavyo ndivyo vinavyounda Chama cha Ushirika cha Mkoa(SIMCU)  wamesema,  wana matumaini makubwa na Chama hicho na wanaamini kitawasaidia katika kuboresha bei ya zao la pamba, kama ilivyoanza kuonekana katika baadhi ya AMCOS wakati wa msimu wa mwaka 2018.

“Tunaimani SIMCU itatusaidia kuimarisha bei ya pamba , mwaka huu bei elekezi ilikuwa 1100/= lakini kupitia mpango wa wenye makampuni kununua kupitia AMCOS baadhi ya maeneo bei iliongezeka ikafikia 1250/=, tunajua viongozi watasimamia tutapata bei nzuri na wakulima tutanufaika kupitia ushirika” alisema Magima Mageme mwanachama kutoa Itilima

“Ushirika ukisimamiwa vizuri unawasaidia wakulima mambo mengi, mwaka huu wakulima walikuwa wanapewa hela zao cash(taslimu) na wanunuzi wa pamba wa makampuni maana hela zote zilikuwa zinaletwa kwenye AMCOS, viongozi wetu tuliowachagua leo watusaidie kusimamia ushirika vizuri” alisema Nkumbamboi Mchunga wa Budalabujiga.

Naye Mrajisi Msaidizi wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Ibrahim Kadudu, amesema Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Simiyu(SIMCU), kitakuwa na wanachama (Vyama vya Ushirika vya msingi (AMCOS) 379, huku akibainisha kuwa AMCOS hizo hadi sasa zimezalisha takribani kilo milioni 100.4 za zao la pamba.

Bw. Kadudu amesema kutokana na uzalishaji huo wa kilo milioni 100.4 za zao la pamba AMCOS zimepata bilioni 3.3 kutokana na ushuru ambao AMCOS inapata shilingi 33/= kwa kila kilo moja ya pamba na Chama cha Ushirika cha Mkoa (SIMCU) kitapokea shilingi Bilioni moja na milioni 40 kutokana na ushuru wa shilingi 10/= katika kila kilo moja ya pamba.

Viongozi wa SIMCU waliochaguliwa ni pamoja na Charles Madata(Mwenyekiti), wajumbe wngine ni Mabula Bwire, Emmanuel Mboi, Simon Magoma, Kulwa Bupuma, Filimoni Sambe na Tuma Magagi.
MWISHO


Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka akizungumza na wanachama wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa huo(SIMCU) katika Mkutano Mkuu wa kwanza, kwa lengo la kuchagua viongozi wa Chama uliofanyika Septemba 04, 2018 Mjini Bariadi, (wa tatu kushoto) Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Dkt. Titus Kamani na wa pili kulia ni Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Simiyu(SIMCU), Bw. Charles Madata . 
Baadhi ya wanachama wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu(SIMCU) wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka katika Mkutano Mkuu wa kwanza wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu(SIMCU), uliofanyika Septemba 04, 2018 Mjini Bariadi kwa lengo la kupata viongozi wa chama hicho.
Mwenyekiti wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika, Dkt. Titus Kamani (kulia) akiteta jambo na Mrajisi Msaidizi wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Ibrahim Kadudu (katikati) mara baada ya Mkutano Mkuu wa kwanza wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu(SIMCU), uliofanyika Septemba 04, 2018 Mjini Bariadi kwa lengo la kupata viongozi wa chama hicho.



Baadhi ya wanachama wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu(SIMCU) wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka katika Mkutano Mkuu wa kwanza wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu(SIMCU), uliofanyika Septemba 04, 2018 Mjini Bariadi kwa lengo la kupata viongozi wa chama hicho.
Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Simiyu, Bw. Ibrahim Kadudu (kulia) akipokea maelekezo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa huo Mhe. Anthony Mtaka, katika Mkutano Mkuu wa kwanza wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu(SIMCU), uliofanyika Septemba 04, 2018 Mjini Bariadi kwa lengo la kupata viongozi wa chama hicho.


0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!