Tuesday, September 25, 2018

VIFO VYA WATOTO WACHANGA VYAPUNGUA SIMIYU


Vifo vya Watoto Wachanga mkoani Simiyu vimepungua kutokana na Serikali kutoa elimu ya uzazi na wazazi kuanza kujifungulia katika vituo vya kutolea huduma ya afya.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi, Katibu wa Wakunga mkoani humo Daud Marwa alisema vifo vimepungua kutokana na jamii kuanza kujenga tabia ya kujifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya.

Alisema kwa mkoa wa Simiyu mwaka 2016 walizaliwa watoto 47,193 lakini waliokufa walikuwa 655, mwaka 2017 walizaliwa watoto 38,442 na walikufa watoto 617 huku mwaka huu wamezaliwa watoto 37,098 na hadi Septemba wamefariki watoto 290.

“Vifo vya Watoto Wachanga mkoani Simiyu vimepungua kutoka 617 mwaka 2017 na kufikia 290 hadi mwezi septemba mwaka huu kutokana serikali kutoa elimu ya uzazi na wazazi kuanza kujifungulia katika vituo vya kutolea huduma ya afya, hii ni jitihada kubwa sana kwani wakunga wamekuwa wakipatiwa mafunzo mara kwa mara, pia kuongezewa stadi za kumhudumia mama na mtoto mwenye uhitaji pindi anapozaliwa’’ alisema Marwa.

Aliongeza kuwa timu ya watumishi wa afya inaendelea kufanya ufuatiliaji na usimamizi ili kuhakikisha kila mama mjamzito anajifungua salama na mtoto mchanga anaendelea kuishi akiwa salama.

Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Mkunga Okoa Maisha Martha Rimoy alisema akinamama wajawazito wengi wao wanapoteza maisha kutokana na kutoka damu nyingi kabla ya kujifungua, wakati wa kujifungua na baada ya kujifungua.

Alisema wanawake 556 kati ya vizazi hai 100,000 hufariki dunia kila mwaka kutokana na kutokwa damu wakati wa kujifungua na kifafa cha mimba, uzazi pingamizi, na uambukizo.

Aliongeza kuwa kutokana na takwimu hizo, hali ya vifo vya wakinamama na watoto wachanga  bado ni mbaya sana hivyo serikali, wadau wa maendeleo na wananchi wanatakiwa kupiga vita vifo hivyo.

Aidha,  katibu huyo alisema baadhi ya wanawake mkoani Simiyu bado wanajifungulia majumbani kutokana na kuwepo kwa wakunga wa jadi na akabainisha kuwa wanaendelea kutoa elimu kwa wakina mama ili waache tabia hiyo badala yake wajifungulie katika vituo vya kutolea huduma za afya ili kuepuka vifo vinavyoweza kuzuilika.

‘’Tunaendelea kutoa elimu kwa wakunga wa jadi na wakinamama wajawazito ili wakipata matatizo ambayo yanazuilika waweze kuwahi vituo vya kutolea huduma za afya, kutoa mafunzo kwa watoa huduma na pia kuboresha sehemu za kutolea huduma’’ alisema Martha Rimoyi.

Naye Katibu Mkuu wa chama cha Wakunga nchini ambaye pia ni Mwalimu wa Wakunga chuo kikuu cha afya na sayansi shirikishi (MUHAS) Dkt. Sebalda Leshabari alisema kazi ya mkunga ni kumshauri mama mjamzito juu ya masuala ya uzazi hadi anapojifungua, lakini kazi ya muuguzi ni kuhudumia mgonjwa.

Alisema wakunga ni watu wenye taaluma ya ukunga na wenye stadi za kuhudumia mama mjamzito, wenye kugundua viashiria vya hatari kwa wajawazito na kutoa rufaa tofauti na wakunga wa jadi ambao hawana taaluma yoyote.

‘’Wakunga wa jadi hawana stadi na utaalamu pindi mama mjamzito anapokuwa na dalili za kushindwa kujifungua salama, hivyo tunawaomba wakinamama wajawazito wajenge tabia ya kujifungulia kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya ili kuzuiwa vifo visivyokuwa vya lazima’’ alisema Dkt. Leshabari.

Semina hiyo ya siku moja kwa waandishi wa Habari mkoa wa Simiyu ililenga kuwajengea uelewa na kufahamu juu ya mkunga, muuguzi na mkunga wa jadi kupitia mradi wa Mkunga Okoa Maisha unaolenga kupunguza vifo vya akinamama wajawazito na watoto wachanga.
MWISHO.



Katibu wa Chama cha Wakunga Tanzania, Dkt. Sebalda Leshabari akizungumza na waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu katika semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi.
Mratibu wa Mradi wa Mkunga Okoa Maisha Martha Rimoy akizungumza na waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu katika semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi.
Katibu wa Wakunga mkoani Simiyu Daud Marwa(kulia) na baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu wakimsikiliza Katibu wa Chama cha Wakunga Tanzania, Dkt. Sebalda Leshabari katika semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi.
Baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu wakifuatlia mada mbalimbali zilizowasilishwa katika semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi.
Baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu wakifuatlia mada mbalimbali zilizowasilishwa katika semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi.

Baadhi ya waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu wakifuatlia mada mbalimbali zilizowasilishwa katika semina ya Mkunga Okoa Maisha iliyofanyika mwishoni mwa wiki jana mjini Bariadi.

0 comments:

Post a Comment

Kumbukumbu za Blogu

Powered by Blogger.
Subscribe Via Email

Subscribe to our newsletter to get the latest updates to your inbox. ;-)

Your email address is safe with us!